Skip to content

Maalim Seif achukuwa fomu kuwania Urais 2020

MJINI UNGUJA: Mwenyekiti wa chama cha ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad, amekabidhiwa rasmi fomu ya kuomba ridhaa kukiwakilisha chama chake kwenye kuwania kiti cha urais wa Zanzibar kwa uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020.

Makamu huyo mstaafu wa rais wa Zanzibar alikabidhiwa fomu hiyo leo Jumaapili (Julai 5) na Katibu Mkuu wa chama hicho, Ado Shaibu, katika ofisi za ACT-Wazalendo zilizopo Vuga, Mjini Unguja.

Akisindikizwa na mamia ya wafuasi wake waliojazana nje na ndani ya ofisi hizo zilizopo Mji Mkongwe, Maalim Seif alisema kwamba endapo chama chake kitamteuwa kuwania wadhifa huo wa juu kwenye serikali ya Zanzibar, ataendeleza ahadi yake ya mwaka 2015 – kuigeuza Zanzibar kuwa Singapore ya Afrika Mashariki.

Hata hivyo, Maalim Seif, ambaye kama akipitishwa atakuwa anawania nafasi hiyo kwa mara ya sita mfululizo, alisema kuchukuwa kwake fomu hiyo hakumaanishi kwamba milango imefungwa kwa wanachama wengine wenye nia ya kuwania wadhifa huo.

Katibu Mkuu Ado Shaibu alisema kwamba pazia limeshafunguliwa rasmi tangu tarehe 1 Julai na kuwatolea wito wote wanaotaka kuwania nafasi kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020 kujitokeza bila kusita na kwamba “kila mtu atapewa fursa sawa kama wengine.”

Leave a Reply