Ishangia Ramadhani
Ishangia Ramadhani, nianze fanya hashuo
Nijiweke kiblani, hijifanya mwanachuo
Ilhali ni shetani, nawavua watu nguo
Ikingia Ramadhani, mimi hujifanya mwema
Nikalisha majirani, wanyonge na mayatima
Japokuwa maluuni, hukaa hashika tama
Hujifanya Muungwana, wachafu nikawabeza
Haacha mambo ya lana, hakaa nikijiliza
Himuomba Maulana, anitoe kwenye giza
Hujileta redioni, nikitoa mawaidha
Hisema huko peponi, kuna mengi yenye ladha
Wakati kwangu moyoni, Ramadhani kubwa adha
Kuna siku hujitowa, nende kuwaona watu
Na vitende nikagawa, wanione nami mtu
Japo nishawapotowa, utu wao sasa butu
Nikiipata nafasi, ya kusema mitaani
Hukumbatia upesi, japo sina jambo geni
Hazungumza kifusi, na mambo yaso thamani
Mimi huwa ninafunga, kwa kuwa nionekane
Kwa kuwa nisipofunga, wataniona mwengine
Kisha wanipige panga, wanizike Meli Nne
Mussa Shehe
27 Mei 2017
Zanzibar
Categories