Umma usiposema… March 13, 2007
Posted by Mohammed Khelef Ghassani in Culture.add a comment
Na Ally Saleh
Wajinga ndio waliwao
Waswahili walisema…
Sijui kama huo msemo
Wanao…maana mimi
Siku nyingi duniani nimehama
Na yalioko huko sinayo
Na ndipo wafanyao
Wanapovinjari na jeuri
Wengineo wanatizama
Wanyonge na wamekosa ari
Kwa vitendo na zao kalima
Mapuuza…wakifanya
Si letu?
Wengineo huo wasema
Letu sote basi nalitote
Umma hausemi
Maana kwa ujinga
Husema…kifo cha jamaa… (more…)
*Mkapa, ukiringia kukingiwa kifua na watawala, kuna wananchi wenye nchi yao March 13, 2007
Posted by Mohammed Khelef Ghassani in Uncategorized.add a comment
Akakumbuka kiburi chake cha uraisi kwa kuwakemea wale ‘wanaomsemasema’ sasa. Kwa kuwa, kwa siku za karibuni, Mkapa amekuwa akisemwa kuhusu kashfa ya ununuzi wa Rada na kwa kuwa tunaomsema ni wananchi, tukiwemo wanahabari (japokuwa mwenyewe alitaka ionekane kwamba ‘wanaomkera’ hivyo ni wapinzani wake wa kisiasa tu), hapa tuseme wazi kwamba hatukuridhika na kemeo lile.
Ametuchefua; na ametukumbusha kuwa yeye hakuwa rais wa kusikiliza malalamiko ya wananchi. Hata akiambiwa watu wameuawa, kama sio watu wa karibu yake kwa mambo yanayomkereketa, sio tu kwamba aliipuzia, bali alihakikisha mfanyaji hapati tatizo lolote. Kwa mfano, kuna yale mauaji ya kutisha yaliyofanywa na Polisi kule Pemba dhidi ya raia zaidi ya 45 wasio na hatia. Alichofanya Mkapa ni kuhakikisha kuwa, waliofanya mauaji yale hawachukuliwi hatua yoyote ya kisheria.
Kwa kipindi cha miaka 10 ya urais wake, nchi hii ilishuhudia ukandamizaji mkubwa wa sauti za umma na demokrasia. Hakuna uchaguzi hata mmoja uliofanywa katika kipindi chake ukawa angalau na asilimia 40% ya uhuru na wa haki ya kweli. Ndiye Mkapa huyo huyo aliyekwenda Zanzibar katika viwanja vya Lumumba mwaka 1996 kuwaambia Wazanzibari ‘wamkome’ kumpelekea barua za kumtaka kushughulikia hali mbaya ya kisiasa na mateso ya Serikali dhidi ya raia hao. Akasema kwamba yeye ni CCM na serikali ni ya CCM. Hataishughulikia wala hatoshughulishwa.
Ndio maana Mkapa sasa anasema hashughulishwi na maneno ya wananchi. Anajua ni yale yale: yeye ni CCM, Rais Jakaya Kikwete na serikali ni CCM; na CCM wana tabia ya kulindana. Labda ndio Kikwete anasema aachwe Mkapa apumzike, asisumbuliwe. Ulinzi huo anaanza kupewa na mwenyewe kauona. Ameanza kujivunia mkoani Pwani.
Hatutaki kuhesabu tena na tena kila kibaya alichokifanya Mkapa kwa nchi hii, lakini tunataka tuseme kwamba huyu bwana aliboronga sana. Si uchuro kumtaka sasa ajibu shutuma na lawama zinazomkabili. Ana mengi ya kujibu kuhusu zahma za Zanzibar katika kipindi cha utawala wake akiwa Amiri Jeshi Mkuu wa nchi.
Kwa mfano, wakati wa kampeni mpaka upigaji kura, Zanzibar aliigeuza Darfur kwa kupeleka majeshi, wengine hata Kiswahili hawajui, kazi yao ni vitisho na kupiga watu tu. Historia ya Zanzibar sasa inaingiza mkasa mpya wa Mtendeni Siege ambapo Wazanzibari walizingirwa katika eneo lote la Makao Makuu ya Chama cha Wananchi (CUF) kwa muda wa siku nne wakiwa na funga ya Ramadhani.
Kwa Jamhuri ya Muungano, ana mengi pia ya kujibu kuhusiana na hilo la Rada na la ndege ya kifahari. Serikali yake iliitumbukiza nchi katika lindi kubwa la ufukara, licha ya kelele za wananchi na nasaha zao kwake. Hakujali. Hakubalilisha msimamo wake na wa chama chake dhidi ya matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi wa nchi hii.
Ni Mkapa, alipokuwa Rais, aliyepewa dhamana katika mikataba hewa na mibovu, ununuzi wa vifaa vibovu na bei ghali wakati huku elimu ikiwa duni, wanafunzi kusoma chini ya miti kwa kukosa vikalio, walimu wenye ujuzi na ukosefu wa madarasa, na huku akiwa na msaada wa mamilioni ya MMEM na MMES.
Sasa ameondoka na ameiacha nchi maskini zaidi kuliko alivyoikuta kutokana na tabia yake mbaya ya kiutawala. Mali ya nchi inakwenda kuwanufaisha watu wa nje, sisi wenyewe tumo kwenye adha chungu nzima za kukosa maji, umeme wa uhakika, barabara mbovu za vijijini na, juu ya yote, ukosefu wa usalama.
Alipokuwa madarakani alijifanya si mtu wa kuambiwa akasikiliza. Na sasa anataka tusimuulize. Basi hata kwa pesa zetu alizozikusanya kwa jasho letu na kodi zetu na kuzigeuza kama mali yake? Alipokuwa madarakani, tulimwambia, hakutaka kusikia. Leo amestaafu, baada ya kuboronga kote huko, halafu anataka bado tuendelee kunyamaza tu, kwa sababu Bwana Kikwete atasema asishughulishwe?
Basi tunamwambia, Kikwete ni Rais wetu sote. Kama ni kuingia madarakani, ni kwa kura zetu sisi, wananchi. Hivyo, hata yeye anawajibika kwetu. Hawezi kutufunga midomo tusiulizie hela yetu. Vyenginevyo, naye aamue kukaa madarakani kwa staili zile zile za kwako, za kimkapamkapa.
Kwa hivyo, tujibu hoja zetu: Ni vipi rada imeingia kwenye rushwa kiasi hiki? Ukiacha ile bei ‘halali’ mulouziana, kile cha juu kiko wapi? Ni vipi ulipitisha mikataba mibovu ya madini? Na, juu ya yote, ni kwa nini watu wengi waliuawa kwa risasi bila ya hatia, tena kwa silaha zilizonunuliwa kwa pesa za walipa kodi wa Tanzania? Tunataka majibu na sio ugeuke mbogo kwa ukali, Mheshimiwa Rais Mstaafu.
Maisha, zama na zamu March 13, 2007
Posted by Mohammed Khelef Ghassani in Uncategorized.add a comment
Mohammed Ghassani
Nilizaliwa mnyonge
Nikakulia unyonge
Lakini
Nilipambana niishi
Niishi waishivyo watu
Watu waitwao watu
Nami nikajikuta
Katika mpambano huo
Naingia ulingoni
Nikarusha makonde
Nami harushiwa pia
Kwamba ndivyo maisha yalivyo
Maisha zama na zamu
Nakumbuka
Mtaa nalozaliwa
Uliitwa Kisiwandui
Zama hizo zikiitwa
Za usultani
Kwetu tulikuwa masikini
Lakini hatukufa njaa
Senti kumi na tano
Nilizopewa na mama
Kununua maandazi
Na uji wa mbaazi
Zilitosha sana
Mimi naye tukaishi
Maisha zama na zamu
Nakumbuka
Nilioshea harita
Ama sabuni ya chokaa
Lakini
Sikuwa mchafu
Wala sikunuka kikwapa
Kwa kuwa usafi wa nguo
Na uswafihi wa nyoyo
Ilikuwa ni khulka
Ya nyumbani
Zanzibari
Mambo ni zama na zamu
Nyumbani?
Ndiyo nyumbani
Japo kwa maana ndogo
Ya kwamba Mola Jalali
Alinijaalia
Nizaliwe Zanzibari
Na pano pawe ni petu
Wazungu huita home
Bahati mbaya ingawa
Waja watawala waovu
Walitaka kwa yakini
Nife na hali si kwetu
Ati niwe stateless
Hawakuweza
Nilikufa Mzanzibari
Kama nalivyozaliwa
Maisha zama na zamu.
Nakumbuka
Kisiwandui yetu
Ya ‘mabondia’ wa mitaani
Akina Msafiri Rocki
Ya Ba Manga na Kaiza
Wekuwa wakipigana
Utadhani wauwana
Hakuna kuamuliza
Ukiingia katikati
Konde mzigo mzima
Vimulimuli machoni
Mbio mtindo mmoja
Maisha zama na zamu.
Nakumbuka
Maduka ya mtaani
Kwa Baba Hadi
Majani ya chai pesa mbili
Sukari pesa nne
Mkate wa pesa sita
Kwa Bi Buluu samaki
Kwa Bi Makiya mbaazi
Maisha zama na zamu.
Nakumbuka
Kisiwandui kuna misikiti
Mmoja tuliuita Makuti
Mwengine Mabati
Nilisali ndani yake
Nikasujudi kwa Mola
Kwamba nami nalikuwa
Dhaifu mbele ya Bwana
Kama walivyo waja wengine
Wajuao Mungu wao
Maisha zama na zamu.
Nawakumbuka
Wanawake wa kikwetu
Walikuwa na heshima
Wakivaa mitandio
Wakijipamba kwa liwa
Kung’arisha ngozi zao
Wakinukia marashi
Na udi wa mawaridi
Nakumbuka kila kitu
Kilichopita maishani
Na hapa sasa nakiri
Maisha zama na zamu.
11 Machi, 2007
Tupumbazeni kwa Popo Bawa, lakini siku moja itakuwa kweli March 13, 2007
Posted by Mohammed Khelef Ghassani in Uncategorized.add a comment
Kwa kawaida, kuna vitu ambavyo huleta pumbazo la akili. Hivi ni vile vinavyoweza kumpelekea mwanadamu kupumbazika na akaweza kuyasahau baadhi ya mambo ambayo yamemzonga na kuisumbua akili yake. Vipumbazio hivi vinajumuisha michezo, vilevi na hata mikusanyiko ya kawaida au ile ya kisiasa. Ukweli ni kuwa haviliondoshi tatizo husika, lakini humfanya mwenye tatizo apumbazike na asahau angalau kwa muda mfupi.
Katika maeneo mengi ya jiji letu la Dar es salaam ni kitu cha kawaida kuwaona wazee au vijana wapo kwenye vijiwe vya karata, bao, draft au viwanja vya mpira, hata mchana wa saa sita. Wakati mwingine watu hawa hudiriki kujitwisha mizigo ya karata za zamani vichwani mwao mithili ya wehu au huamua kucheza mpira mchana, wakati jua lipo utosini.
Hali hii mara nyingi husababishwa na kutokuwa na shughuli ya maana ya uzalishaji na kuweza kujiingizia kipato. Ni hali ambao husababisha tafrani (frustration) na hupelekea mtu kukata tamaa, na kwa wengine kuwa ndio mwanzo wa kujiingiza kwenye vitendo viovu kama vya wizi, ukahaba na utumiaji wa kupindukia wa pombe na madawa ya kulevya.
Ni katika vijiwe na viwanja hivi ambamo mambo mengi hujadiliwa (kwa maana yetu ya mitaani ya mjadala). Khabari za fulani kafumaniwa au idadi ya vimada alivyonavyo, humu ndio mahala mwake. Au kuwakuta vijana wakibishana kuhusu utajiri wa Salim Bakhresa na Mohamed Dewji, hilo ni jambo la kawaida katika maeneo haya. Ni nadra kusikia mambo ya maana.
Lakini, kwa siku za karibuni, imeanza kutokezea kuwa katika sehemu hizi ndimo ambamo lawama na uoza dhidi ya serikali iliopo madarakani zinamozungumzwa na kusikika kwa sauti ya juu kupita ile ya redio. Maeneo haya ndio ambayo pia wanasiasa wajanja hupenda kuyatumia ili kufikia malengo yao ya kisiasa. Si kitu cha ajabu kuona mwanasiasa akigawa maboksi ya karata au mpira na jezi pindi anapohitaji kura za kuingia madarakani. Hii ni kwa sababu mengi wa watumiaji wa maeneo haya ni watu wenye uelewa au elimu ndogo kuhusu mambo mbalimbali.
Lakini pia, maeneo haya ni muafaka kwa watu wa Usalama na wale maajenti wa kuwazuga watu ili mambo mabaya na kashfa nyingine ambazo zinaiandama serikali zisahaulike vichwani mwa watu. Na mara nyingi hawa watu wa vijiweni ndio ambao hutumika kama makasuku wa kusambaza taarifa hizo za kubuniwa bila wenyewe kijijua.
Kwa mara ya kwanza baada ya kumalizika uchaguzi mkuu wa raisi, wabunge na madiwani wa mwaka 1995, ndio lilipoibuniwa suala hili la Popobawa. Kwa wakati ule liliibuliwa kisiwani Pemba.
Itakumbukwa kwamba uchaguzi wa Zanzibar wa mwaka 1995 uligubikwa ni hujuma mbali mbali, wizi na ukiukwaji mkubwa wa haki za binaadamu. Ni uchaguzi ambao hata wafadhili waliupigia kelele na wakakatisha misaada yao kwa Zanzibar. Wakati suala la Zanzibar kutengwa ni jumuia za kimataifa likifukuta, ndipo ghafla lilipobuniwa suala hili la Popo Bawa.
Mengi yalisikika kuhusiana na Popo hilo, lakini kitu cha kushangaza ni kwamba hakuna mtu ambae aliwahi kujitokeza au ambaye watu waliwahi kumuona na kuthibitisha kwamba aliwahi kufanyiwa kitendo cha kulawitiwa, ambacho jini huyo anadaiwa kuwafanyia wanadamu, kinyume na inavyodaiwa na watu kwamba pindi jini huyo anapokulawiti ni lazima utangaze.
Wakati suala hili halikuweza kuwapumbaza wananchi wale wa Pemba, ambao kwa wakati huo walikua kwenye madhila na manyanyaso makali kutoka kwa watawala, cha kushangaza ni kwamba kwa kiasi kikubwa hili lilifanikiwa kuzipumbaza akili za watu wengi ambao walikuwa wakipata taarifa kupitia magazeti ya udaku yalioamua kuzishabikia taarifa hizo kwa dhumuni la kuuza biashara yao zaidi.
Mara baada ya maajenti wa usambazaji wa hizi taarifa za Popo Bawa kushindwa kuzipumbaza akili za Wazanzibari, ndipo wakaibuka na jingine: kwamba Wapemba walikua wanapakaza vinyesi kwenye mashule na kwenye visima vya maji ya kunywa. Lakini tujiulize, je inawezekana kwa mtu mwenye akili timamu kuweka kinyesi kwenye maji au majengo ya shule ambayo mwanawe anayatumia?
Kwa wale wasioifahamu Pemba, wanaweza kusumbuka kupata picha halisi. Lakini ukweli ni kwamba, hadi wakati huo, maeneo mengi ya kisiwa cha Pemba hayajafikiwa na maji ya bomba, badala yake maji yanayotumika ni maji ya visima vifupi au vile vya kutumia kamba. Na mara nyingine visima hivi huwa si zaidi ya kimoja kwa kila kijiji. Sasa vipi mtu mwenye akili timamu aweze kukihujumu kile ambacho hana mbadala nacho?
Vibweka na viroja hivi havikuishia hapo, kwani mara tu baada ya uchaguzi wa mwaka 2005, na ambao, kama kawaida, ulishuhudia pia uvunjaji mwengine mkubwa wa haki za binadamu ambao ulisimamiwa na kuratibiwa na vyombo vya dola kwa upande wa Zanzibar, ghafla likaibuka pumbazo jipya. Hili likawa pumbazo la keki kujiandika maandishi ya Kiarabu yaliyomtaja Mwenyezi Mungu (S.W) au Mtume Muhammad (S.A.W).
Ni mapumbazo ambayo mara zote kwa Zanzibar yamekuwa yakibuniwa wakati ambao jamii inakuwa kwenye lindi la machafuko na huzuni. Kwa bahati nzuri, ni kuwa mara zote ambazo mapumbazo haya yamekuwa yakibuniwa, Wazanzibari wameweza kuwa makini na wagumu wa kutolewa kwenye fikra za kutoyafikiria matatizo yanayowasibu. Wamekuwa bado wakiiona mitego iliyobuniwa na wajanja kuwasahaulisha watu ili wasiyazungumze wala kuyajadili mambo maovu yanayofanywa na wale walio madarakani kwa maslahi yao binafsi.
Katika miezi ya hivi karibuni, vyombo vingi vya habari vimekuwa vikizungumzia matatizo mbalimbali yanayoikabili nchi yetu kwa upana wake na bila ya woga. Mengi yamezungumzwa na kuandikwa na pia kuhojiwa na vyombo hivyo. Hii ni baada ya kujitokeza kwa masuala mazito ambayo ni dhahiri kwamba utekelezaji wake una walakini mkubwa na ambao kwa sasa unaitafuna na kuigharimu nchi yetu. Masuala kama ya rada, ambayo inadaiwa kwamba wajanja wametafuna bilioni kumi na mbili pesa za walipa kodi wanyonge wa Tanzania, pamoja na masuala ya mikataba mibovu ya kuingamiza nchi, ndege mbovu ya raisi ambayo pia ina harufu ya rushwa na migomo ya wanafunzi wa vyuo vikuu dhidi ya bodi ya mikopo isiyokwisha, haya yote yanaiandama serikali na ndio yaliyotawala vichwa vya Watanzania wengi.
Ghafla limeibuka tena pumbazo la “Popo Bawa kaingia Dar anafanya vitu vyake.” Watu wanazikimbia nyumba zao kwa vile wanamuogopa Popo Bawa huyo. Wanaibuka wanaojiita watabiri na waganga maarufu kwenye vyombo vya habari, nao wanazungumzia Popo Bawa! Kibaya zaidi ni kwamba watabiri na waganga hao maarufu, wanamnasibisha huyo Popo Bawa wao waliyembuni na watu wa jamii ya Kipemba.
Kama nilivyoeleza kwamba, mara zote ambazo mapumbazo haya yamekuwa yakibuniwa, Wazanzibari wameweza kuwa makini na daima wamekuwa wakicheza ndani ya lindi la matatizo yanayowasibu na sio kwenye mitego iliyobuniwa na wajanja kwa lengo la kuwasahaulisha. Hawajapata kuacha kuzungumzia wala wala kuyajadili mambo maovu yanayofanywa na wale walio madarakani kwa maslahi yao binafsi.
Kutokana na magazeti mengi ya udaku na ambayo yanapendwa na wasomaji wengi kushabikia uzushi huu, mitaani nako kila upitapo kuanzia masokoni, vijiweni, viwanjani mpaka nyumbani, ni khabari za Popo Bawa. Popo Bawa tu!
Ni dhahiri kwamba sasa ngoma imepata wapigaji na wachezaji. Watu hawana tena muda wa kufikiria na kujadili kuhusu tatizo la umeme wa Richmond, wala suala la rada pamoja na ndege mbovu ya Raisi. Wamezugwa wamezugika!
Hayati Bob Marley aliwahi kutahadharisha, ingawa watu wengi wanadai kwamba aliimba. Bob alitahadharisha kwa kusema: You can fool some people sometime. But you can’t fool all the people all the time. Akimaanisha kwamba: “Unaweza kuwadanganya baadhi ya watu kwa wakati fulani. Lakini huwezi kuwadanganya watu wote muda wote.” Haya ni maneno aliyozungumza Bob, ambaye kuna watu kwao ni mvuta bangi asiye na maana.
Imewezekana leo kupumbaza watu hawa kwa pumbazo la Popo Bawa. Kesho mnaweza pia kuwapumbaza kwa kuwaambia kwamba “Real Madrid wanakuja Tanzania” hata kama ujio huo hautoshibisha matumbo yao wala kuondoa dhiki walizonazo, zaidi ya kuligharimu Taifa hili mnalodai maskini mabilioni ya pesa.
Lakini kuna siku wataamka kama walivyokwishaamka wale wa Zanzibar, na watahoji. Sasa ikijakufikia hatua hiyo, muwe na jibu la kuja kuwapa, kwani mapumbazo ya kitoto hayatowanusuru na hayatofua dafu mbele ya ghadhabu watakazo kuwa nazo. Na wale wasanii wabunifu wa wimbo wa Popo Bawa, hawatokua tena na wimbo wala mziki wa kuwatuliza mzuka wao wa mabadiliko utakaokuwa umekwisha panda. Kuna siku itakuwa kweli, chembilecho mpenzi wetu, Marehemu Ali Nabwa. Na hiyo siku haiko mbali hivyo.
abdullahahmad21@yahoo.com
Simu Na. 0717 198980
She Can and Is Everything March 8, 2007
Posted by Mohammed Khelef Ghassani in Uncategorized.add a comment
A poem on Women’s Day by Mohammed Ghassani
Look around you
At your back, at your front
At your left, at your right
Can’t you see Her?
Yes,
Here She Is
Here, there and everywhere
And in you yourself
You feel Her presence
And
Her very existence
She, a Woman
It’s all about women!
Those people you see
Their houses you admire
Their cars you grasp
Their lives they enjoy
All
Possible have been made
Enabled
By Her
It’s all about woman!
You know:
As child we speak those first words
They are named: motherence
As we grow speaking that first language
They call it
Mother language
Our in-born intellect
Mothertec, so it’s known
They all come from
Our mothers
From women
It’s all about woman!
Women have ever since
Brought us to this world
Nurtured us with their kindness
Taught us with their knowledge
They can, therefore,
Do anything else
They are, therefore,
Everything else
It’s all about women!
We, men are
Nothing but images
Of theirs
Their success
Their happiness and
Pride
It’s all about women!
As bad as sometimes we become
Their failures
Their atrocities
But
No matter what
They never give up
Praises be to the Lord
For creating these creatures
The women
Because
It’s all about women!
8th March, 2007
Dar es Salaam